Monday, February 16, 2015

Panga pangua ya ratiba Ligi Kuu ni aibu kwa TFF

ad300
Advertisement

Jamal Malinzi,Rais wa TFF. PICHA|MAKTABA

Tangu Ligi Kuu ya Tanzania Bara ianze Septemba mwaka jana, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF)  limekuwa likiipangua ratiba yake kwa sababu mbalimbali.
Sababu hizo ni viwanja wanavyokuwa wamepanga kuvitumia kwa ajili ya ligi hiyo kuhitajika kwa shughuli nyingine za kisiasa, maandalizi ya timu ya Taifa, maombi binafsi ya dharura ya timu hivyo kubadilisha tarehe ya mechi na Kombe la Mapinduzi.
Kutokana na sababu hizo, TFF imekuwa ikilazimika kujikuta mara kwa mara ikibadilisha ratiba yake ya Ligi Kuu.
Mabadiliko hayo ni kama maji yaliyokwisha kumwagika kwani yameshafanyika na ligi inaendelea. Lakini yameacha athari kubwa na ndiyo maana tunataka suala la mabadiliko ya ratiba lishughulikiwe haraka na TFF ili kulipunguza au kulimaliza kabisa.
Inafahamika wazi kwamba kabla ya ligi kuanza, TFF hupata nafasi ya kuandaa kalenda yake ya matukio ya mwaka mzima na kuipeleka Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na vyama vya soka vya mikoani kufahamu kalenda hiyo.
Vyama vya soka mikoani ndiyo vinavyofanya kazi ya kuomba matumizi ya viwanja husika mikoani hivyo kama TFF ilipanga ratiba yake ya matukio msimu huu bila kuangalia ratiba za shughuli kubwa za kisiasa za nchi, matamasha mbalimbali na shughuli nyingine za michezo, lazima hilo litawapa tabu viongozi wa vyama vya soka mikoani.
Upangaji wa ratiba ya ligi kubwa na muhimu kama hiyo unahitaji umakini wa hali ya juu. Haipendezi hata kidogo kuona kila mara inafanyiwa marekebisho. Tungependa kuona ratiba ambayo angalau inatekelezeka kwa asilimia zaidi ya 80 bila kufanyiwa marekebisho.
Tunasema walau kwa asilimia 80 tukitilia maanani ugumu uliokuwapo katika upangaji ratiba kwani ni dhahiri kwamba miundombinu yetu ya nchi na matukio mengine, hayawezi kukwepeka.
Lakini suala kama ratiba ya ligi kuingiliwa na mechi za kimataifa ni uzembe kwa kuwa siyo mambo yanayozuka ghafla. Mechi hizo au tarehe zake zinafahamika vyema ni suala la umakini tu.
 Mbali na hilo, jambo jingine linalotushangaza ni kuona kwamba yanapofanyika marekebisho ya ratiba yanatolewa bila kuonyesha mabadiliko yaliyofanyika na ratiba mpya itakavyokuwa.
Hivi sasa tumekuwa tukitumiwa barua pepe na Ofisa Habari wa TFF kwamba mechi za wiki hii za Ligi Kuu ya Vodacom ni kama ifuatavyo; Februari  21- Mbeya City vs Yanga,  Kagera Sugar vs JKT Ruvu,  Mgambo Shooting vs Mtibwa Sugar, Feb 22- Stand United vs Simba,  Azam vs Tanzania Prisons. Februari 25- Mbeya City vs Ruvu Shooting.
Tunaamini kwamba kama TFF ingekuwa makini katika suala hili la Katiba, mosi isingeruhusu kuwa na viraka vingi, lakini pili ingekuwa na mabadiliko machache ambayo yangetoa fursa kwa wadau kuyafahamu kirahisi na kujipanga kwa maana ya timu kujiandaa na mashabiki pia.
Tunasema hivyo kwa sababu hivi sasa ni rahisi kuwa na ratiba sahihi ya Ligi ya England, Ujerumani, Italia na Hispania kuliko kuwa na ratiba sahihi ya mechi zijazo ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
Tunaamini kuwa mashabiki wa soka wa Tanzania wanapenda kuona ratiba sahihi ya mechi zijazo za Ligi Kuu ya Tanzania Bara na takwimu nyingi zinazohusu ligi hiyo.
Tunatarajia TFF itatoa ratiba mpya na kupunguza kutengeneza ratiba ambayo itakuwa inapanguliwa mara kwa mara ili ligi hiyo siyo tu kwamba isikose mvuto, bali kuepuka kero na aibu hii.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 Post a Comment: